Ezekieli 7:1-27
7 Neno la Yehova likanijia tena likisema:
2 “Nawe Mwana wa binadamu, hivi ndivyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anavyoiambia nchi ya Israeli: ‘Mwisho! Mwisho umezifikia pembe nne za nchi.
3 Sasa mwisho umekufikia, nami nitakumwagia hasira yangu, nami nitakuhukumu kulingana na njia zako na kukuadhibu* kwa sababu ya matendo yako yote yanayochukiza.
4 Jicho langu halitakusikitikia; wala sitakuhurumia,+ kwa maana nitakuletea matokeo ya njia zako mwenyewe, nawe utapatwa na madhara ya matendo yako yanayochukiza.+ Nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’+
5 “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Tazama! Msiba, msiba wa pekee, unakuja.+
6 Mwisho unakuja; mwisho utakuja; utainuka* wenyewe dhidi yako. Tazama! Unakuja.
7 Zamu yako imefika,* wewe unayekaa nchini. Wakati unakuja, siku hiyo iko karibu.+ Kuna vurugu, wala si kelele za shangwe milimani.
8 “‘Hivi karibuni nitakumwagia ghadhabu yangu,+ nami nitakumwagia hasira yangu yote,+ nami nitakuhukumu kulingana na njia zako na kukuadhibu* kwa sababu ya matendo yako yote yanayochukiza.
9 Jicho langu halitakusikitikia; wala sitakuhurumia.+ Kwa maana nitakuletea matokeo ya njia zako mwenyewe, nawe utapatwa na madhara ya matendo yako mwenyewe yanayochukiza. Nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi, Yehova, ndiye ninayewapiga.+
10 “‘Tazama, ile siku! Tazama, inakuja!+ Zamu yako imefika;* fimbo imechanua na kimbelembele kimechipuka.
11 Ukatili umesitawi na kuwa fimbo ya uovu.+ Wao wenyewe, mali yao, umati wao, wala umashuhuri wao hautaokoka.
12 Wakati utakuja, siku hiyo itafika. Mnunuzi asishangilie, na muuzaji asiomboleze, kwa maana kuna ghadhabu dhidi ya umati wao wote.*+
13 Kwa maana muuzaji hatakirudia kitu alichouza, hata uhai wake ukiokolewa, kwa maana maono hayo yanahusu umati wote. Hakuna atakayerudi, na kwa sababu ya kosa lake,* hakuna atakayeokoa uhai wake.
14 “‘Wamepiga tarumbeta+ na kila mtu yuko tayari, lakini hakuna anayeenda vitani, kwa sababu nina ghadhabu dhidi ya umati wote.+
15 Upanga uko nje,+ na ugonjwa hatari na njaa kali zimo ndani. Yeyote aliye uwanjani atakufa kwa upanga, na njaa kali na ugonjwa hatari vitawameza wale walio jijini.+
16 Watu wao watakaofanikiwa kuponyoka wataenda milimani, na kama njiwa wa mabondeni, kila mmoja ataomboleza kwa sababu ya kosa lake.+
17 Mikono yao yote italegea, na magoti yao yote yatadondosha maji.*+
18 Wamevaa nguo za magunia,+ nao wanatetemeka.* Kila mtu ataaibishwa, na kila kichwa kitakuwa na upara.*+
19 “‘Watatupa fedha yao barabarani, nayo dhahabu yao itawachukiza. Wala fedha yao wala dhahabu yao haitaweza kuwaokoa katika siku ya ghadhabu ya Yehova.+ Hawatashiba,* wala kuyajaza matumbo yao, kwa maana vitu hivyo* vimekuwa kikwazo kinachosababisha kosa lao.
20 Walijivunia urembo wa mapambo yao, nao wakayatumia* kutengeneza mifano yao inayochukiza, sanamu zao zinazochukiza.+ Ndiyo sababu nitaifanya fedha na dhahabu yao kuwa chukizo kwao.
21 Nami nitaitia* mikononi mwa wageni ili waipore na kuwapa waovu wa dunia kuwa nyara, nao wataitia unajisi.
22 “‘Nami nitaugeuza uso wangu kutoka kwao,+ nao watapatia unajisi mahali pangu palipofichika,* na wanyang’anyi wataingia mahali hapo na kupatia unajisi.+
23 “‘Tengeneza mnyororo,*+ kwa maana nchi imejaa hukumu yenye madoa ya damu+ na jiji limejaa ukatili.+
24 Nami nitaingiza mataifa mabaya kabisa,+ nayo yatamiliki nyumba zao,+ nami nitakikomesha kiburi cha wenye nguvu, na mahali pao patakatifu patatiwa unajisi.+
25 Maumivu yao yatakapokuja, watatafuta amani lakini haitakuwepo.+
26 Msiba utakuja juu ya msiba, na habari baada ya habari, na watu watatafuta maono kutoka kwa nabii,+ lakini sheria itatoweka* kutoka kwa kuhani na ushauri* kutoka kwa wazee.+
27 Mfalme ataomboleza,+ naye mkuu atavaa kukata tamaa,* na mikono ya watu wa nchi itatetemeka kwa hofu. Nitawatendea kulingana na njia zao, nami nitawahukumu kama walivyohukumu. Nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’”+
Maelezo ya Chini
^ Au “kukufanya uwajibike.”
^ Tnn., “utaamka.”
^ Au labda, “Shada lako la maua limefika.”
^ Au “kukufanya uwajibike.”
^ Au labda, “Shada lako la maua limefika.”
^ Yaani, wale wanaonunua mali na pia wale wanaouza hawatafaidika, kwa maana wote wataangamizwa.
^ Au labda, “kwa kosa lake.”
^ Yaani, watajikojolea kwa sababu ya woga.
^ Yaani, vichwa vyao vitanyolewa kwa sababu ya maombolezo.
^ Tnn., “wamefunikwa na hofu.”
^ Au “Nafsi zao hazitashiba.”
^ Yaani, fedha yao na dhahabu yao.
^ Yaani, mapambo ya dhahabu na fedha.
^ Yaani, fedha yao na dhahabu yao waliyotumia kutengeneza sanamu.
^ Inaonekana ni sehemu ya ndani zaidi ya mahali patakatifu pa Yehova.
^ Yaani, minyororo ya utekwa.
^ Au “mafundisho yatatoweka.”
^ Au “mashauri.”
^ Au “ukiwa.”