SOMO LA 84
Yesu Anatembea Juu ya Maji
Zaidi ya kuwaponya wagonjwa na kuwafufua wafu, Yesu alikuwa na uwezo wa kudhibiti dhoruba na mvua. Baada ya kusali pale mlimani, Yesu aliona dhoruba kwenye Bahari ya Galilaya. Mitume wake walikuwa kwenye mashua wakijitahidi kupiga makasia licha ya dhoruba kali. Yesu alishuka kutoka mlimani na kuanza kutembea juu ya maji akielekea kwenye mashua yao. Mitume walipomwona mtu akitembea juu ya maji, waliogopa sana. Lakini Yesu akawaambia hivi: ‘Ni mimi, msiogope.’
Petro akasema: ‘Bwana, ikiwa kweli ni wewe, niamuru nije kwako.’ Yesu akamwambia Petro: ‘Njoo.’ Kwa hiyo, dhoruba ilipokuwa ikiendelea, Petro akatoka kwenye mashua na kuanza kutembea juu ya maji kumwelekea Yesu. Lakini, alipomkaribia Yesu, Petro akaitazama ile dhoruba, akaogopa na kuanza kuzama. Petro akapaza sauti: ‘Bwana, niokoe!’ Yesu akamshika mkono, na kumuuliza: ‘Kwa nini umeingiwa na shaka? Imani yako iko wapi?’
Yesu na Petro wakaingia kwenye mashua, na mara moja ile dhoruba ikatulia. Wazia jinsi mitume walivyohisi! Walisema hivi: “Kwa kweli wewe ni Mwana wa Mungu.”
Huu haukuwa wakati pekee ambao Yesu alidhibiti hali ya hewa. Wakati fulani Yesu alipokuwa pamoja na mitume wake wakivuka kuelekea upande ule mwingine wa bahari, Yesu alilala usingizi kwenye mashua. Alipokuwa amelala, dhoruba kali ikatokea. Mawimbi yakaipiga mashua, nayo ikajaa maji. Mitume wakamwamsha Yesu wakisema hivi kwa sauti kubwa: ‘Mwalimu, tunakaribia kufa! Tusaidie!’ Yesu akaamka na kuiambia hivi bahari: “Nyamaza!” Mara moja, upepo ukaacha kuvuma na bahari ikatulia. Yesu akawauliza hivi mitume: ‘Imani yenu iko wapi?’ Wakaanza kuzungumza wenyewe kwa wenyewe wakisema: “[Hata] upepo na bahari vinamtii.” Mitume walijifunza kwamba ikiwa watamtegemea Yesu kikamili, hawatahitaji kuogopa kitu chochote.
“Ningekuwa wapi ikiwa singekuwa na imani kwamba nitauona wema wa Yehova katika nchi ya walio hai?”—Zaburi 27:13