Mathayo 27:1-66
27 Asubuhi ilipofika, wakuu wote wa makuhani na wanaume wazee wa watu wakashauriana juu ya Yesu ili auawe.+
2 Na, baada ya kumfunga, wakampeleka na kumtia mkononi mwa gavana Pilato.+
3 Ndipo Yuda, aliyemsaliti, alipoona kuwa amekwisha kuhukumiwa adhabu, akajuta, akavirudisha vile vipande 30+ vya fedha kwa wakuu wa makuhani na wanaume wazee,
4 akisema: “Nilitenda dhambi niliposaliti damu yenye uadilifu.”+ Wakasema: “Hilo linatuhusu nini? Shauri yako!”+
5 Basi akatupa vile vipande vya fedha hekaluni akaondoka, akaenda zake akajinyonga.+
6 Lakini wakuu wa makuhani wakavichukua hivyo vipande vya fedha na kusema: “Si halali kuvitumbukiza katika hazina takatifu, kwa sababu hivyo ni bei ya damu.”
7 Baada ya kushauriana pamoja, wakavitumia kununua shamba la mfinyanzi ili kuzikia wageni.
8 Kwa hiyo shamba hilo limeitwa “Shamba la Damu”+ mpaka leo hii.
9 Ndipo likatimizwa lililosemwa kupitia nabii Yeremia, akisema: “Nao walichukua vile vipande 30 vya fedha,+ ambavyo ni bei juu ya mtu aliyepigwa bei, ambaye baadhi ya wana wa Israeli walimpigia bei,
10 nao wakavitoa kwa ajili ya shamba la mfinyanzi,+ kulingana na lile ambalo Yehova alikuwa ameniamuru.”
11 Yesu sasa akasimama mbele ya gavana; naye gavana akamuuliza: “Je, wewe ndiye mfalme wa Wayahudi?”+ Yesu akajibu: “Wewe mwenyewe unasema.”+
12 Lakini, alipokuwa akishtakiwa+ na wakuu wa makuhani na wanaume wazee, hakujibu.+
13 Ndipo Pilato akamwambia: “Je, husikii ni mambo mangapi wanashuhudia juu yako?”+
14 Lakini hakumjibu, hata neno moja, hivi kwamba gavana akastaajabu sana.+
15 Sasa kutoka sherehe mpaka sherehe ilikuwa desturi ya gavana kufungulia umati mfungwa mmoja, ambaye walimtaka.+
16 Wakati huohuo walikuwa wamemshika mfungwa mwenye sifa mbaya anayeitwa Baraba.+
17 Kwa sababu hiyo walipokuwa wamekusanywa pamoja Pilato akawaambia: “Mnataka niwafungulie nani, Baraba au Yesu anayeitwa Kristo?”+
18 Kwa maana alijua kwamba walikuwa wamemtia mikononi mwake+ kwa sababu ya wivu.+
19 Zaidi ya hayo, alipokuwa ameketi juu ya kiti cha hukumu, mke wake akampelekea habari, akisema: “Usijihusishe kamwe na mtu huyo mwadilifu,+ kwa maana niliteseka sana leo katika ndoto+ kwa sababu yake.”
20 Lakini wakuu wa makuhani na wanaume wazee wakaushawishi umati uombe wapewe Baraba,+ lakini Yesu aangamizwe.
21 Sasa gavana akajibu, akawaambia: “Mnataka niwafungulie nani kati ya hawa wawili?” Wakasema: “Baraba.”+
22 Pilato akawaambia: “Basi, nitafanya nini na Yesu anayeitwa Kristo?” Wote wakasema: “Atundikwe mtini!”+
23 Akasema: “Kwani, amefanya jambo gani baya?” Bado wao wakaendelea kupaaza sauti hata zaidi: “Atundikwe mtini!”+
24 Alipoona kwamba haikufaidi kitu bali, badala yake, ghasia zilikuwa zikitokea, Pilato alichukua maji+ na kunawa mikono yake mbele ya ule umati, akisema: “Mimi sina hatia ya damu ya mtu huyu. Shauri yenu.”
25 Ndipo watu wote wakajibu, wakasema: “Damu yake iwe juu yetu na juu ya watoto wetu.”+
26 Ndipo akawafungulia Baraba, lakini akaagiza Yesu apigwe mijeledi+ na kumtoa ili atundikwe mtini.+
27 Ndipo askari-jeshi wa gavana wakampeleka Yesu ndani ya jumba la gavana na kukusanya pamoja kikosi chote cha askari kwake.+
28 Nao wakamvua kanzu yake, wakampamba kwa joho jekundu,+
29 nao wakasokota taji kutokana na miiba na kuliweka juu ya kichwa chake na utete katika mkono wake wa kuume. Nao wakapiga magoti mbele yake, wakamfanyia dhihaka,+ wakisema: “Siku njema, ewe Mfalme wa Wayahudi!”+
30 Nao wakamtemea mate+ na kuuchukua ule utete na kuanza kumpiga kichwani.
31 Mwishowe, walipokuwa wamemdhihaki,+ wakalivua lile joho na kumvika mavazi yake ya nje na kumpeleka akatundikwe mtini.+
32 Walipokuwa wakiondoka walimkuta mzaliwa wa Kirene anayeitwa Simoni.+ Wakamlazimisha aubebe mti wake wa mateso.
33 Nao walipofika mahali panapoitwa Golgotha,+ ndiyo kusema, Mahali pa Fuvu la Kichwa,
34 wakampa divai iliyochanganywa na nyongo+ anywe; lakini, baada ya kuionja, akakataa kuinywa.+
35 Walipokuwa wamemtundika mtini+ wakagawa mavazi yake ya nje+ kwa kupiga kura,+
36 na, huku wakiwa wameketi, wakamlinda hapo.
37 Pia, wakabandika juu ya kichwa chake shtaka juu yake, kwa kuandika: “Huyu ni Yesu Mfalme wa Wayahudi.”+
38 Ndipo wanyang’anyi wawili wakatundikwa mtini pamoja naye, mmoja upande wake wa kuume na mwingine upande wake wa kushoto.+
39 Kwa hiyo wapita-njia wakaanza kumtukana,+ wakitikisa+ vichwa vyao
40 na kusema: “Ewe uliyetaka kuliangusha hekalu+ na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe mwenyewe! Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, shuka kutoka kwenye mti wa mateso!”+
41 Vivyo hivyo pia wakuu wa makuhani pamoja na waandishi na wanaume wazee wakaanza kumfanyia dhihaka na kusema:+
42 “Aliwaokoa wengine; yeye mwenyewe hawezi kujiokoa! Yeye ni Mfalme+ wa Israeli; acheni sasa ashuke kutoka kwenye mti wa mateso nasi tutamwamini.+
43 Ameweka tegemeo lake katika Mungu; acheni Yeye sasa amwokoe+ ikiwa Yeye anamtaka, kwa maana alisema, ‘Mimi ni Mwana wa Mungu.’ ”+
44 Vivyo hivyo hata wanyang’anyi waliotundikwa mtini pamoja naye wakaanza kumshutumu.+
45 Tangu saa sita na kuendelea kukawa na giza+ juu ya nchi yote, mpaka saa tisa.+
46 Karibu saa tisa Yesu akapaaza kilio kwa sauti kubwa, akisema: “Eli, Eli, lama sabakthani?” yaani, “Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniacha?”+
47 Waliposikia hilo, baadhi ya wale waliokuwa wamesimama hapo wakaanza kusema: “Mtu huyu anamwita Eliya.”+
48 Na mmoja wao akakimbia mara moja, akachukua sifongo akailowesha kwenye divai kali+ akaiweka juu ya utete na kuanza kumnywesha.+
49 Lakini wale wengine wao wakasema: “Acha iwe hivyo kwake! Acheni tuone kama Eliya atakuja kumwokoa.”+ [[Mtu mwingine akachukua mkuki na kumchoma ubavuni, na damu na maji vikatoka.]]+
50 Tena Yesu akapaaza sauti kubwa, akaitoa roho yake.+
51 Na, tazama! pazia+ la patakatifu likapasuka vipande viwili, kutoka juu mpaka chini,+ na dunia ikatetemeka, na miamba ikapasuka.+
52 Na makaburi yakafunguka na miili mingi ya watakatifu waliokuwa wamelala usingizi ikainuliwa,
53 (na watu, waliokuwa wakitoka kati ya makaburi baada ya kufufuliwa kwake, wakaingia katika jiji takatifu,)+ nayo ikaonwa na watu wengi.
54 Lakini yule ofisa-jeshi na wale waliokuwa pamoja naye wakimlinda Yesu, walipoona tetemeko la nchi na mambo yaliyokuwa yakitendeka, wakaogopa sana, wakisema: “Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu.”+
55 Zaidi ya hayo, wanawake wengi walikuwa hapo wakitazama wakiwa mbali,+ waliokuwa wamefuatana na Yesu kutoka Galilaya ili kumhudumia;+
56 ambao kati yao alikuwamo Maria Magdalene, pia Maria mama ya Yakobo na Yose, na mama ya wana wa Zebedayo.+
57 Sasa kwa kuwa ilikuwa jioni, mtu mmoja tajiri wa Arimathea, anayeitwa Yosefu, ambaye yeye mwenyewe pia alikuwa mwanafunzi wa Yesu, akaja.+
58 Mtu huyu alimwendea Pilato na kuomba apewe mwili wa Yesu.+ Ndipo Pilato akaamuru apewe huo.+
59 Na Yosefu akauchukua mwili huo, akaufunga katika kitani safi kizuri,+
60 na kuulaza katika kaburi lake jipya,+ alilokuwa amechimba katika mwamba. Na, baada ya kuviringisha jiwe kubwa kwenye mlango wa lile kaburi, akaondoka.+
61 Lakini Maria Magdalene na yule Maria mwingine wakabaki hapo, wakiwa wameketi mbele ya kaburi hilo.+
62 Siku iliyofuata, baada ya yale Matayarisho,+ wakuu wa makuhani na Mafarisayo walikusanyika pamoja mbele ya Pilato,
63 wakisema: “Bwana, tumekumbuka kwamba mjanja huyo alisema alipokuwa bado yuko hai, ‘Baada ya siku tatu+ nitafufuliwa.’
64 Kwa hiyo amuru kaburi lilindwe mpaka siku ya tatu, ili wanafunzi wake wasipate kamwe kuja na kumwiba+ na kuwaambia watu, ‘Alifufuliwa kutoka kwa wafu!’ na ujanja huu wa mwisho utakuwa mbaya zaidi kuliko ule wa kwanza.”
65 Pilato akawaambia: “Ninyi mna walinzi.+ Nendeni mkalilinde jinsi mnavyojua.”
66 Basi wakaenda na kulilinda kaburi kwa kulitia jiwe muhuri+ na kuweka walinzi.

