Kutoka 14:1-31
14 Sasa Yehova akasema na Musa, na kumwambia:
2 “Sema na wana wa Israeli, kwamba warudi na kupiga kambi mbele ya Pihahirothi katikati ya Migdoli na bahari, kukabili Baal-sefoni.+ Mbele yake mtapiga kambi kando ya bahari.
3 Kisha Farao hakika atasema kuhusu wana wa Israeli, ‘Wanatanga-tanga nchini kwa kuvurugika. Nyika imewazingira.’+
4 Kwa hiyo, kwa kweli nitauacha moyo wa Farao uwe mkaidi,+ naye hakika atawafuatilia wao nami nitajipatia utukufu kupitia kwa Farao na majeshi yake yote;+ nao Wamisri watajua hakika kwamba mimi ni Yehova.”+ Basi wakafanya vivyo hivyo.
5 Baadaye mfalme wa Misri akaambiwa kwamba watu walikuwa wamekimbia na kwenda zao. Mara moja moyo wa Farao na watu wake vilevile ukabadilika kuhusiana na watu,+ kwa hiyo wakasema: “Tumefanya nini, kwa kuwaruhusu Waisraeli waende zao, waache kuwa watumwa+ wetu?”
6 Kwa hiyo akatayarisha magari yake ya vita, na kuwachukua watu wake pamoja naye.+
7 Naye akachukua magari mia sita yaliyochaguliwa+ na yale magari mengine yote ya Misri na mashujaa wa vita juu ya kila moja la magari hayo.
8 Basi Yehova akauacha moyo wa Farao mfalme wa Misri uwe mkaidi,+ naye akawafuatilia wana wa Israeli, huku wana wa Israeli wakienda kwa mkono ulioinuliwa.+
9 Nao Wamisri wakawafuatilia, na farasi wote wa magari wa Farao na askari wake wapanda-farasi+ na majeshi yake wakawafikia walipokuwa wamepiga kambi kando ya bahari, karibu na Pihahirothi, kukabili Baal-sefoni.+
10 Farao alipokaribia, wana wa Israeli wakaanza kuinua macho yao, na tazama, Wamisri walikuwa wakipiga mwendo wakiwafuatilia; na wana wa Israeli wakaogopa sana na kuanza kumlilia Yehova.+
11 Nao wakamwambia Musa: “Je, ni kwa sababu hakuna makaburi yoyote huko Misri ndiyo sababu umetuleta hapa ili tufie nyikani?+ Ni nini hiki ambacho umetutendea kwa kutuongoza kutoka Misri?
12 Je, hili silo neno tulilokuambia huko Misri, tukisema, ‘Tuache, tuwatumikie Wamisri’? Kwa maana ni afadhali kwetu tuwatumikie Wamisri kuliko kufa nyikani.”+
13 Kisha Musa akawaambia watu: “Msiogope.+ Simameni imara muuone wokovu wa Yehova, atakaowafanyia ninyi leo.+ Kwa maana Wamisri mnaowaona leo hamtawaona tena, hasha, hamtawaona tena kamwe.+
14 Yehova mwenyewe atawapigania ninyi,+ nanyi wenyewe mtakaa kimya.”
15 Sasa Yehova akamwambia Musa: “Kwa nini unaendelea kunililia?+ Waambie wana wa Israeli kwamba wanapaswa kuvunja kambi.
16 Wewe nawe, inua fimbo+ yako na kuunyoosha mkono wako juu ya bahari, uitenganishe,+ ili wana wa Israeli wapate kupita katikati ya bahari juu ya nchi kavu.+
17 Mimi nami, tazama, nitaiacha mioyo ya Wamisri iwe mikaidi,+ ili waingie kuwafuatilia wao nami nijipatie utukufu kupitia kwa Farao na majeshi yake yote, magari yake ya vita na askari wake wapanda-farasi.+
18 Na Wamisri hakika watajua kwamba mimi ni Yehova nitakapojipatia utukufu kupitia kwa Farao, magari yake ya vita na askari wake wapanda-farasi.”+
19 Ndipo malaika+ wa Mungu wa kweli aliyekuwa akienda mbele ya kambi ya Israeli akaondoka na kwenda nyuma, nayo nguzo ya wingu ikaondoka mbele yao na kusimama nyuma yao.+
20 Kwa hiyo ikaingia katikati ya kambi ya Wamisri na kambi ya Israeli.+ Kwa upande mmoja ikawa wingu pamoja na giza. Kwa upande ule mwingine ikawa ikiuangaza usiku.+ Nacho kikundi hiki hakikukaribia kikundi kile usiku kucha.
21 Sasa Musa akanyoosha mkono wake juu ya bahari;+ naye Yehova akaanza kuifanya bahari irudi nyuma kwa upepo wenye nguvu wa mashariki usiku kucha na kuligeuza bonde la bahari liwe nchi kavu,+ nayo maji yalikuwa yakitenganishwa.+
22 Mwishowe wana wa Israeli wakapita katikati ya bahari juu ya nchi kavu,+ huku maji yakiwa ukuta kwao mkono wao wa kuume na wa kushoto.+
23 Na Wamisri wakaanza kufuatilia, nao farasi wote wa Farao, magari yake ya vita na askari wake wapanda-farasi wakaanza kuingia baada yao,+ kuingia katikati ya bahari.
24 Na ikawa kwamba wakati wa kesha la kuamkia asubuhi, Yehova akaanza kuiangalia kambi ya Wamisri kutoka ndani ya nguzo ya moto na wingu,+ naye akaivuruga+ kambi ya Wamisri.
25 Naye akawa akiyaondoa magurudumu kutoka kwenye magari yao hivi kwamba wakawa wakiyaendesha kwa shida;+ nao Wamisri wakaanza kusema: “Na tukimbie tusikaribie Israeli hata kidogo, kwa sababu hakika Yehova anawapigania dhidi ya Wamisri.”+
26 Mwishowe Yehova akamwambia Musa: “Unyooshe mkono wako juu ya bahari,+ ili maji yarudi juu ya Wamisri, magari yao ya vita na askari wao wapanda-farasi.”
27 Mara moja Musa akaunyoosha mkono wake juu ya bahari, nayo bahari ikaanza kurudia hali yake ya kawaida asubuhi ikikaribia. Wakati wote huo Wamisri walikuwa wakikimbia wasikutane nayo, lakini Yehova akawakung’uta Wamisri katikati ya bahari.+
28 Nayo maji yakaendelea kurudi.+ Mwishowe yakafunika magari ya vita na askari wapanda-farasi wa majeshi yote ya Farao na ambao walikuwa wameingia baharini kuwafuatilia.+ Hakuna hata mmoja kati yao aliyebaki.+
29 Nao wana wa Israeli, walitembea juu ya nchi kavu katikati ya sakafu ya bahari,+ nayo maji yalikuwa kwao ukuta mkono wao wa kuume na wa kushoto.+
30 Basi siku hiyo Yehova akaokoa Israeli kutoka kwa mkono wa Wamisri,+ na Israeli wakawaona Wamisri wakiwa wamekufa kando ya bahari.+
31 Israeli wakauona pia ule mkono mkuu ambao Yehova aliufanya utende juu ya Wamisri; nao watu wakaanza kumwogopa Yehova na kuwa na imani katika Yehova na katika Musa mtumishi wake.+