Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Yeremia 11:11—“Nitaleta Mabaya Juu Yao”

Yeremia 11:11—“Nitaleta Mabaya Juu Yao”

“Kwa hiyo Yehova anasema hivi: ‘Ninawaletea msiba ambao hawataweza kuuepuka. Watakaponiomba msaada, sitawasikiliza.’”​—Yeremia 11:11, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

“Basi, BWANA asema hivi, Tazama, nitaleta mabaya juu yao, ambayo hawataweza kuyakimbia; nao watanililia, lakini sitawasikiliza.”​—Yeremia 11:11, Revised Union Version.

Maana ya Yeremia 11:11

 Mungu alikuwa akizungumza na Wayahudi walioishi katika siku za nabii Yeremia. Kwa kuwa watu walikuwa wakipuuza sheria za uadilifu za Yehova a na mashauri yenye upendo yaliyokuwa yakitolewa na manabii wake, yeye asingewalinda wasipatwe na madhara ya mwenendo wao mbaya.​—Methali 1:24-32.

 “Kwa hiyo Yehova anasema hivi.” Maneno “kwa hiyo” yanahusianisha maneno yanayofuata na mistari inayotangulia. Kwenye Yeremia 11:1-10, Yehova aliwaambia watu wake kwamba walikuwa wamevunja agano, au makubaliano ya kudumu, ambayo mababu zao walikuwa wamefanya pamoja naye. (Kutoka 24:7) Badala ya kumwabudu Muumba wao, Wayahudi walikuwa wakiabudu sanamu. Uasi-imani huo uliongoza kwenye aina zote za uovu—kutia ndani kuwadhabihu watoto!—Yeremia 7:31.

 “Ninawaletea msiba.” Mara nyingi, Biblia inaposema Mungu alifanya jambo, inamaanisha kwamba aliliruhusu litokee. Ilikuwaje hivyo katika kisa hiki? Watu wa Yehova walipoanza kuabudu miungu ya uwongo na kupuuza viwango vyake vyenye manufaa, walijiletea maumivu mengi sana. Pia, walipoteza ulinzi wa Mungu. Kwa sababu hiyo, adui mwenye nguvu, yaani, mfalme wa Babiloni, alifaulu kulishinda Yerusalemu na kuwapeleka wakaaji wake uhamishoni. Miungu ya uwongo ambayo watu walikuwa wameitumaini isingeweza kuwaokoa.​—Yeremia 11:12; 25:8, 9.

 Kwa kuruhusu misiba hiyo iwapate watu wake, Mungu hakuwa akitenda isivyo haki au kwa uovu. Yakobo 1:13 inasema: “Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” Tafsiri ya Revised Union Version inasema kwamba Mungu ‘ataleta mabaya juu ya Wayahudi.’ Hata hivyo, neno la awali b linalotafsiriwa “mabaya” kwenye Yeremia 11:11 linaweza pia kutafsiriwa “msiba” au “maafa”​—maneno ambayo yanafafanua vizuri kuteseka ambako Wayahudi walikabili.

 “Watakaponiomba msaada, sitawasikiliza.” Yehova hasikilizi sala za wale ambao “mikono [yao] imejaa damu” au ambao wanategemea miungu ya uwongo iwaokoe. (Isaya 1:15; 42:17) Hata hivyo, anasikiliza sala za wale ambao wanatubu kikweli kutokana na njia zao mbaya na kumrudia kwa unyenyekevu.​—Isaya 1:16-19; 55:6, 7.

Muktadha wa Yeremia 11:11

 Katika mwaka wa 647 K.W.K., Yehova alimpa Yeremia mgawo wa kuwa nabii wake. Kwa miaka 40, Yeremia aliwaonya watu wa Yuda kuhusu hukumu ya Mungu iliyokuwa ikija. Lakini walikataa kusikiliza. Wakati huo, nabii huyo aliandika maneno yaliyo kwenye Yeremia 11:11. Mwishowe, katika mwaka wa 607 K.W.K., maonyo ya kinabii yalitimizwa wakati ambapo Wababiloni waliangamiza Yerusalemu.​—Yeremia 6:6-8; 39:1, 2, 8, 9.

 Kitabu cha Yeremia kinatia ndani ujumbe wa tumaini. Yehova alisema hivi: “Miaka 70 itakapotimia huko Babiloni . . . nitatimiza ahadi yangu kwa kuwarudisha mahali hapa [nyumbani kwa Wayahudi].” (Yeremia 29:10) Yehova ‘alitimiza’ ahadi hiyo mwaka wa 537 K.W.K., Wamedi na Waajemi walipowashinda Wababiloni. Yehova aliwaruhusu watu wake, waliokuwa wamesambaa kotekote katika milki hiyo, warudi nyumbani na kurudisha ibada ya kweli.​—2 Mambo ya Nyakati 36:22, 23; Yeremia 29:14.

 Tazama video hii fupi inayoonyesha muhtasari wa kitabu cha Yeremia.

a Yehova ndilo jina linalotumiwa kwa kawaida katika Kiswahili kuwakilisha herufi nne za Kiebrania zinazoashiria jina la kibinafsi la Mungu. Ili ufahamu kwa nini tafsiri nyingi za Biblia zinatumia jina la cheo “Bwana” badala ya jina la kibinafsi la Mungu, ona makala yenye kichwa “Yehova Ni Nani?

b Maandiko ya Kiebrania, ambayo mara nyingi yanajulikana kama Agano la Kale, yaliandikwa katika Kiebrania na Kiaramu.