Hamia kwenye habari

Kwa zaidi ya miaka 70, gazeti Mnara wa Mlinzi limepatikana katika Kizulu

FEBRUARI 1, 2024
AFRIKA KUSINI

Kutangaza Ufalme wa Yehova Katika Kizulu kwa Miaka 75

Kutangaza Ufalme wa Yehova Katika Kizulu kwa Miaka 75

Kufikia Januari 2024, miaka 75 imepita tangu Mnara wa Mlinzi lianze kuchapishwa kwa mara ya kwanza katika Kizulu. Kuanzia mwaka wa 1949, nakala za Mnara wa Mlinzi za Kizulu zilichapishwa katika ofisi ya tawi ya Afrika Kusini kwa kutumia mashine za uchapishaji zilizoendeshwa kwa mikono. Baadaye, ofisi ya tawi ilipata mashine za kisasa za uchapishaji, na hivyo kutokeza magazeti mengi na bora zaidi.

Mtafsiri katika miaka ya 1980 akitumia mashine kutafsiri machapisho yanayotegemea Biblia katika Kizulu

Mwanzoni haikuwa rahisi kupata mahali panapofaa pa kulala kwa ajili kikundi cha watafsiri wa Kizulu. Hali hiyo ilisababishwa na sheria za ubaguzi nchini Afrika Kusini ambazo ziliwazuia watu weupe na weusi kuishi katika jengo moja. Ndugu na dada weusi waliotafsiri Kizulu walilazimika kuishi kwenye majengo yaliyokuwa nje ya Betheli. Kwa sababu hiyo, mara nyingi walilazimika kutumia muda mwingi kusafiri kufika ofisini, na hilo liliongeza gharama na matatizo mengine. Kwa mfano, pindi fulani, watafsiri 20 wa Kizulu, waliishi katika chumba kimoja cha kulala. Ndugu Alfred Phatswana alikuwa mmoja wa wale waliovumilia hali hiyo ngumu, kwa muda wa miaka miwili kuanzia mwaka wa 1981. Leo, akiwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Afrika Kusini, anakumbuka hivi: “Haikuwa rahisi kuishi kwenye chumba hicho. Hata hivyo, tulifurahi kwamba tulikuwa na mahali pa kuishi ili kuunga mkono kazi ya utafsiri. Kwa kuongezea, kwa kuwa tulihakikisha kwamba maeneo hayo tuliyoishi yalikuwa safi muda wote, hilo lilitoa ushahidi mzuri.”

Tunafurahi kwamba sasa ndugu na dada zetu wanaweza kukaa pamoja katika majengo yenye starehe ya ofisi ya utafsiri ya Durban, Afrika Kusini. Sasa zaidi ya wahubiri 28,000 katika makutaniko 584 ya Kizulu wanaendelea kunufaika kupitia gazeti la Mnara wa Mlinzi na machapisho mengine yanayotegemea Biblia katika lugha yao wenyewe.

Picha ndogo juu: Ofisi ya utafsiri (RTO) iliyo jijini Durban, Afrika Kusini. Picha ndogo chini: Baadhi ya ndugu na dada wanaotumikia katika ofisi ya utafsiri (RTO). Kulia: Ndugu na dada wakihubiri habari njema kwa kutumia Mnara wa Mlinzi katika Kizulu

Tunashangilia kwamba Yehova anaendelea kubariki kazi ya wale wanaotafsiri Mnara wa Mlinzi na machapisho mengine yanayotegemea Biblia katika Kizulu ili wengi zaidi ‘wachukue maji ya uzima bure.’​—Ufunuo 22:17.