1 Samweli 9:1-27
9 Basi palikuwa na mtu wa Benyamini, na jina lake lilikuwa Kishi,+ mwana wa Abieli, mwana wa Zerori, mwana wa Bekorathi, mwana wa Afia, Mbenyamini,+ mtu mwenye nguvu ya mali.+
2 Naye alikuwa na mwana ambaye jina lake lilikuwa Sauli,+ kijana na mwenye sura nzuri, wala hakuwako mwanamume yeyote wa wana wa Israeli aliyekuwa na sura nzuri kuliko yeye; kutoka kwenye mabega yake kwenda juu alikuwa mrefu kuliko watu wote.+
3 Na punda-jike+ za Kishi baba ya Sauli wakapotea. Basi Kishi akamwambia Sauli mwana wake: “Tafadhali, chukua pamoja nawe mmoja wa watumishi, uondoke, uende kuwatafuta hao punda-jike.”
4 Naye akaenda, akipita katika eneo lenye milima la Efraimu,+ akaendelea, akapita katika nchi ya Shalisha,+ wala hawakuwapata. Nao wakaendelea, wakapita katika nchi ya Shaalimu, lakini hawakuwa huko. Naye akaendelea, akapita katika nchi ya Wabenyamini, wala hawakuwapata.
5 Nao wakaingia katika nchi ya Sufu; na Sauli akamwambia mtumishi wake aliyekuwa pamoja naye: “Haya njoo, turudi, ili baba yangu asije akaacha kufikiri juu ya punda-jike na kuanza kuhangaika juu yetu.”+
6 Lakini yeye akamwambia: “Tafadhali, tazama! Kuna mtu wa Mungu+ katika jiji hili, na mtu huyo anaheshimiwa. Kila jambo analosema hutimia bila kukosa.+ Na twende huko sasa. Labda anaweza kutuambia njia yetu tunayopaswa kuiendea.”
7 Ndipo Sauli akamwambia mtumishi wake: “Na tukienda, tutampelekea mtu huyo nini?+ kwa maana mkate umekwisha katika vyombo vyetu, wala hakuna zawadi+ yoyote ya kumpelekea huyo mtu wa Mungu wa kweli. Tuna nini pamoja nasi?”
8 Basi mtumishi akamjibu Sauli tena na kusema: “Tazama! Kuna sehemu ya nne ya shekeli+ ya fedha mkononi mwangu, nami nitampa huyo mtu wa Mungu wa kweli, naye atatuambia njia yetu.”
9 (Nyakati za kale katika Israeli, mtu alikuwa akisema hivi akienda kumtafuta Mungu: “Haya njooni, na twende kwa mwonaji.”+ Kwa maana nabii wa leo alikuwa akiitwa mwonaji nyakati za kale.)
10 Ndipo Sauli akamwambia mtumishi wake: “Neno lako ni jema.+ Haya njoo, twende.” Nao wakaenda zao kwenye jiji lile alilokuwamo mtu wa Mungu wa kweli.
11 Walipokuwa wakipanda kwenda jijini, wakakuta wasichana wakitoka kwenda kuteka maji.+ Basi wakawauliza: “Je, mwonaji+ yuko mahali hapa?”
12 Nao wakawajibu na kusema: “Ndiyo. Tazama! Yuko mbele yenu. Fanyeni haraka sasa, kwa sababu amekuja jijini leo, kwa maana leo kuna dhabihu+ kwa ajili ya watu katika mahali pa juu.+
13 Mara mtakapoingia jijini, mtamkuta moja kwa moja kabla hajapanda kwenda mahali pa juu ili ale chakula; kwa kuwa watu hawawezi kula mpaka aje, kwa maana yeye ndiye anayeibariki dhabihu.+ Baadaye wale walioalikwa hula. Basi sasa pandeni—sasa hivi mtampata.”
14 Nao wakapanda kwenda jijini. Walipokuwa wakiingia katikati ya jiji, tazama, Samweli alikuwa anatoka nje kuja kuwapokea ili kupanda kwenda mahali pa juu.
15 Naye Yehova alikuwa amefunua sikio+ la Samweli ile siku iliyotangulia kuja kwa Sauli, akisema:
16 “Karibu wakati kama huu kesho nitatuma mtu kwako kutoka katika nchi ya Benyamini,+ nawe umtie mafuta+ awe kiongozi juu ya watu wangu Israeli; naye atawaokoa watu wangu kutoka mkononi mwa Wafilisti,+ kwa sababu nimeona mateso ya watu wangu, kwa maana kilio chao kimenifikia.”+
17 Na Samweli akamwona Sauli, naye Yehova akamjibu: “Huyu ndiye mtu niliyekuambia, ‘Huyu ndiye atakayewazuia watu wangu wasipite mipaka.’”+
18 Ndipo Sauli akamkaribia Samweli katikati ya lango na kusema: “Tafadhali niambie, Nyumba ya mwonaji iko wapi?”
19 Naye Samweli akamjibu Sauli na kusema: “Mimi ndiye mwonaji. Panda mbele yangu, uende mahali pa juu, nanyi mtakula pamoja nami leo,+ nami nitawaacha mwende zenu asubuhi, nami nitakuambia mambo yote yaliyo moyoni mwako.+
20 Na wale punda-jike uliowapoteza siku tatu zilizopita,+ usitie moyo+ wako juu yao, kwa maana wamepatikana. Na je, vitu vyote vyenye kutamanika vya Israeli ni vya nani?+ Je, si vyako na vya nyumba yote ya baba yako?”
21 Ndipo Sauli akajibu na kusema: “Je, mimi si Mbenyamini wa kutoka katika kabila dogo zaidi+ kati ya makabila ya Israeli,+ na je, familia yangu si dhaifu zaidi kati ya familia zote za kabila la Benyamini?+ Basi kwa nini umeniambia jambo kama hili?”+
22 Ndipo Samweli akamchukua Sauli na mtumishi wake, akawaleta katika jumba la kulia chakula, akawapa viti mbele+ ya wale walioalikwa; nao walikuwa karibu watu 30.
23 Baadaye Samweli akamwambia mpishi: “Leta lile fungu nililokupa, ambalo juu yake nilikuambia hivi, ‘Liweke kando yako.’”
24 Kwa hiyo yule mpishi akainua ule mguu na ile nyama iliyokuwa juu yake, akauweka mbele ya Sauli. Naye akasema tena: “Kilichowekwa akiba ndicho hiki. Kiweke mbele yako. Ule, kwa maana wamekuwekea hicho akiba mpaka wakati uliowekwa ili ule pamoja na wale walioalikwa.” Basi Sauli akala pamoja na Samweli siku hiyo.
25 Kisha wakashuka kutoka mahali pa juu,+ wakaenda jijini, naye akaendelea kusema na Sauli darini.+
26 Nao wakaamka mapema na ikawa, mara kulipopambazuka, Samweli akamwita Sauli juu darini, akisema: “Simama, nikuache uende zako.” Basi Sauli akasimama na wote wawili, yeye na Samweli, wakatoka nje.
27 Walipokuwa wakishuka ukingoni mwa jiji, Samweli akamwambia Sauli: “Mwambie mtumishi+ apite mbele yetu”—basi akapita—“nawe simama tuli sasa ili nikuambie neno la Mungu.”