1 Samweli 11:1-15
11 Na Nahashi Mwamoni+ akapanda na kupiga kambi juu ya Yabeshi+ katika Gileadi. Kwa hiyo watu wote wa Yabeshi wakamwambia Nahashi: “Fanya agano pamoja nasi ili tukutumikie.”+
2 Ndipo Nahashi Mwamoni akawaambia: “Nitafanya agano pamoja nanyi kwa sharti hili, kwa sharti la kung’oa+ kila jicho lenu la kuume, nami ni lazima niweke jambo hilo kuwa shutuma juu ya Israeli wote.”+
3 Nao wanaume wazee wa Yabeshi wakamwambia: “Tupatie muda wa siku saba, nasi tutatuma wajumbe katika eneo lote la Israeli, na, ikiwa hatutapata mwokozi,+ ndipo tutalazimika kuja kwako.”
4 Baadaye hao wajumbe wakaja Gibea+ la Sauli na kusema maneno hayo masikioni mwa watu, na watu wote wakaanza kupaaza sauti zao na kulia.+
5 Lakini tazama, Sauli akija nyuma ya mifugo yake kutoka shambani, naye Sauli akasema: “Watu wana nini, kwamba walie?” Wakaanza kumsimulia maneno ya wale watu wa Yabeshi.
6 Na roho+ ya Mungu ikaanza kutenda kazi juu ya Sauli alipoyasikia maneno hayo, hasira yake ikawaka sana.+
7 Kwa hiyo akachukua ng’ombe-dume wawili, akawakata vipande-vipande, akavipeleka katika eneo lote la Israeli+ kwa mkono wa wajumbe, akisema: “Yeyote kati yetu ambaye hatatoka akiwa mfuasi wa Sauli na Samweli, ng’ombe zake watafanywa hivi!”+ Na hofu+ ya Yehova+ ikaanza kuwashika watu hivi kwamba wakatoka kama mtu mmoja.+
8 Ndipo akahesabu+ watu hao katika Bezeki, na wana wa Israeli wakawa jumla ya 300,000, na watu wa Yuda 30,000.
9 Basi wakawaambia wale wajumbe ambao walikuwa wamekuja: “Hivi ndivyo mtakavyowaambia watu wa Yabeshi katika Gileadi, ‘Kesho mtapata wokovu wakati wa jua kali.’”+ Basi wale wajumbe wakaja na kuwaambia watu wa Yabeshi, nao wakaanza kushangilia.
10 Kwa hiyo watu wa Yabeshi wakasema: “Kesho tutawajia ninyi, nanyi mtutendee kulingana na yote yaliyo mema machoni penu.”+
11 Na ikawa kesho yake kwamba Sauli+ akaweka watu katika vikosi vitatu;+ nao wakaingia katikati ya kambi wakati wa kesha la kuamkia asubuhi+ na kuwapiga Waamoni+ mpaka wakati siku ilipokuwa na jua kali. Na baadhi yao walipoonekana kuwa wamebaki, ndipo wakatawanywa, wala hawakubaki watu wawili wakiwa pamoja kati yao.+
12 Na watu wakaanza kumwambia Samweli: “Ni nani wanaosema, ‘Je, Sauli atakuwa mfalme juu yetu?’+ Watoeni watu hao, ili tuwaue.”+
13 Hata hivyo, Sauli akasema: “Mtu yeyote asiuawe leo,+ kwa maana leo Yehova ametimiza wokovu katika Israeli.”+
14 Baadaye Samweli akawaambia watu: “Njooni, twende Gilgali,+ ili tuufanye upya ufalme huko.”+
15 Basi watu wote wakaenda Gilgali, kisha wakamfanya Sauli kuwa mfalme mbele za Yehova katika Gilgali. Ndipo wakatoa huko dhabihu za ushirika mbele za Yehova,+ na Sauli na watu wote wa Israeli wakaendelea kushangilia huko kwa hali ya juu sana.+